Ulezi ni jukumu kubwa ambalo linapaswa kuchukuliwa mtu anapokuwa tayari, kihisia, kifedha na kiakili. Katika umri huu ambapo mambo mengi yanafanyika na kuzinduliwa kwenye mtandao, ni rahisi sana kwa watoto kupata ujumbe hata wasiofaa kujua katika umri mchanga. Vidokezo vya ulezi wa kidijitali ni muhimu kwa wazazi wote.
Kuwa mzazi kunahitaji juhudi na wakati mwingi. Hata baada ya kutia juhudi na kumlea mtoto kwa njia ipasayo, huenda akafanya vitu ambavyo vitakuwa na athari hasi kwake. Mara nyingi, mzazi hana usemi wala nguvu za kubadilisha haya.
Hata hivyo, kuna vidokezo ambavyo wazazi wanaowalea watoto katika kipindi hiki cha dijitali wanaweza kutumia.
Vidokezo vya ulezi wa kidijitali

- Sisitiza nidhamu
Wafunze watoto wako kuhusu mazuri na mabaya na usiogope kuwapatia nidhamu wanapokosea. Nidhamu sio kitu ambacho unafunza mtoto mara moja. La, unamfunza na kusisitiza kila mara. Ni muhimu watoto wanapojua kuwa kila tendo lina athari, chanya ama hasi na wawe tayari kupatiwa nidhamu wanapokosea.
Kuchapa watoto kumepitwa na wakati. Njia kama kuwazungumzia, kuondoa haki za kutazama runinga baada ya kukosea ama hata kutocheza na marafiki zao ni baadhi ya njia za kuwapa nidhamu.
2. Kuwa na urafiki wa karibu na watoto wako

Ni muhimu kwa wazazi kutenga muda wa kuwa na watoto wao. Mbali na wakati wa kila siku unapowasaidia kufanya kazi za ziada ama kuwalisha. Hakikisha kuwa unapata wakati wa kuzungumza nao. Kuwajulia hali, walivyoshinda shuleni, walichosoma, kilichofanyika walipokuwa shuleni. Pia, hakikisha kuwa unazungumza kuhusu mambo yanayofanyika maishani mwako, vitu vinavyokusumbua ili wafahamu kuwa ni kawaida kutatizika na wanaweza kueleza wanapokuwa wakipitia mambo magumu.
3. Wafunze kuhusu elimu ya kingono
Katika kipindi hiki cha kidigitali, watoto wanaweza kupata ujumbe kuhusu kufanya mapenzi kwa urahisi. Kupitia kwa mitandao ya kijamii ama marafiki zao. Kwa sababu hii, ni muhimu kwa mzazi kuhakikisha kuwa mafunzo kuhusu ngono yanatoka kwake kwanza. Mafunzo haya yatakuwa ya kweli, utangamano kati ya mzazi na mtoto utaongezeka na mtoto atawasiliana na mzazi wakati wote anapokuwa na matatizo katika sekta hiyo maishani mwake.
4. Kuwa makini na watu wanaohusiana na watoto wako
Marafiki, majirani na wanajamii wanaohusiana na mtoto wako huwa na kiwango cha athari maishani mwao. Hakikisha kuwa unajua mambo wanayozungumzia wanapokuwa pamoja. Wafunze watoto wako kuzungumza mtu anapojaribu kuwashika kwa njia isiyofaa.
5. Dhibiti utumiaji wa simu

Hapo awali, ilikuwa vigumu kwa wanafunzi kuwa na simu. Ila sasa, watoto walio darasa la tatu wana simu. Huenda ikawa vigumu kumnyima mtoto wako simu. Ikiwa utampatia simu, hakikisha kuwa unadhibiti wakati anaotumia simu na apps zilizo kwenye simu yake.
Chanzo: Healthline
Soma Pia: Tiba za Kinyumbani za Maumivu ya Kichwa Unazopaswa Kujua